shuku image TIA MBEYA

Wednesday, May 16, 2012

Zijue taratibu za kuanzisha biashara

na shukran mwakisu
Wapendwa wasomaji ni wiki nyingine tena kama ada tuanze kwa kumshukuru Mungu kutujalia uhai. Napenda kutumia fursa hii kuwashawishi baadhi ya watu wanaofikiria kuanzisha biashara.
Bila shaka endapo msomaji  anafanya biashara atakuwa   amepata mambo matatu ambayo yatakusaidia kurekebisha mahali ambako ulikosea.

Je, ni njia zipi unapaswa kupitia ili kuwa mjasiriamali? Hili ni swali  gumu sana kwa sababu majibu yanatofautiana.
Kama hujawahi kufikiria kuwa mjasiriamali na inatokea bahati mbaya unatafuta kazi, lakini hujapata na ukaamua kuanzisha biashara utakuwa katika wakati mgumu kupata mafanikio.

Lakini kwa mtu mwingine ambaye amekuwa akifikiria kuwa mjasiriamali, hakika ukianza biashara utakuwa katika nafasi nzuri ya kufanikiwa.
Zifuatazo ni mbinu za kuwa mjasiriamali bora:
1. Elimu: Pata taarifa mbalimbali za ujasiriamali fahamu faida na changamoto. Pia fahamu tabia za wajasiriamali waliofanikiwa ujenge taswira ya mjasiriamali wa namna gani utakuwa. Mathalani kama bado uko shule au chuo hudhuria vipindi vingi vya elimu ya ujasiriamali.
Kama hauko shule, tafuta namna yoyote upate elimu mfano elimu ya watu wazima, makongamano, warsha, midahalo, mafunzo, kuangalia televisheni na sikiliza redio. Angalizo: jipangie muda maalumu ili usitumie muda mwingi kujifunza na kuchelewa kuanza biashara. Suala la elimu linaendelea hata baada ya kuanzisha biashara.
2. Jenga ndoto kubwa: Katika hatua nyingine ili kuwa mjasiriamali bora, weka mikakati ya kwamba unataka kuwa mjasiriamali wa aina gani. Fikiria miaka mitano, kumi mpaka 20 itakuaje. Pia fikiria namna gani utaiendesha biashara ya ndoto yako.
Katika hatua hii usisumbuke kufikiria namna ya kupata fedha ya kuanzisha biashara. Kama utaanza kuwa na wasiwasi wapi utapata fedha, pia hutaweza kuanza biashara.
Katika hatua hii, wasiliana na watu mbalimbali wenye biashara, waulize walianzaje. Pia fikiria mambo makubwa. Usiwaze kufanya vitu vidogo ambavyo kila mtu anaweza kufanya.
3. Mipango: Baada ya kujenga ndoto yako, andika mipango mbalimbali jinsi ya kuanzisha biashara. Mipango hii sio mchanganuo wa biashara bali andika mambo mbalimbali unayojifunza kutoka kwa wajasiriamali wenzako na tunza vizuri taarifa hizo.
Kama umenunua gazeti na kuona habari njema kwako chana kipande na tunza, inapendeza ukiwa na faili au hata bahasha fulani hivi tunza vipande vya karatasi unazoandika mambo yako siku moja utaifungua na utagundua una taarifa nyingi za kukusaidia kuanzisha biashara.
4. Fedha: Vyanzo vya fedha ni akiba kwa mjasiriamali. Kama umeajiriwa kopa kwa ajili ya biashara, pia pokea msaada kutoka kwa wazazi, ndugu jamaa au rafiki. Wakati mwingine unaweza kutafuta wawekezaji kama biashara ni kubwa. Kwa msaada zaidi tembelea ‘smallbusinessfinancing.com’.
5. Maandalizi: Baada ya hatua hizo  fanya maandalizi, fanya mchanganuo kujua wateja wako ni nani, wanapenda nini, uwezo wao wa kununua. Jipange namna gani taarifa zitawafikia endapo utaanzisha biashara.
Biashara ni matangazo. Pia kama utahitaji wafanyakazi, ni muda mwafaka kuchanganua utaanza na wangapi kwa nafasi zipi. Fikiria zaidi mahitaji ya biashara unayotarajia kuanzisha kwa mfano leseni, vibali na  eneo la biashara.

6. Anzisha biashara: Baada ya mipango na maandalizi kukamalika unashauriwa kuanzisha biashara. Tangaza biashara yako, fanya  tafrija fupi, karibisha familia, jamaa na marafiki ili wajue biashara yako.
Katika tafrija hiyo unaweza kupata wateja au mtandao wa biashara yako. Unaweza kuanzia hapo.
7. Fanya marekebisho ya mipango: Wahenga walisema mipango sio matumizi kwa kuwa inawezekana  kabisa uliyoyapanga kabla ya kuanza biashara, yakawa tofauti.
Kutokana na hali hiyo chukua fursa ya kufanya marekebisho haraka iwezekanavyo na kuboresha maeneo yenye mahitaji.
+255753 686 848

No comments:

Post a Comment