shuku image TIA MBEYA

Friday, May 4, 2012

Baraza jipya la mawaziri: Mawaziri sita watimuliwa

  Sura mpya tatu zajitokeza
  Manaibu Waziri 2 nje, 10 wapya
Rais Jakaya Kikwete amewafukuza kazi mawaziri sita waliotuhumiwa kukiuka maadili ya utumishi na kushiriki ubadhirifu wa mali za umma.
Mawaziri hao na Wizara zao kwenye mabano ni Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii), Cyril Chami (Viwanda na Biashara) na Omar Nundu (Uchukuzi).
Wengine ni Dk Haji Mpanda (Afya na Ustawi wa Jamii), William Ngeleja (Nishati na Madini) na Mustapha Mkulo (Fedha).
Kwenye orodha ya waliofutwa kazi wamo Naibu Mawaziri, Dk Lucy Nkya (Afya na Ustawi wa Jamii) na Athuman Mfutakamba (Uchukuzi).
Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya:
Kwa upande wa mawaziri wapya ni Dk Abdallah Kigoda (Viwanda na Biashara), William Mgimwa (Fedha) na Profesa Sospeter Muhogo (Nishati na Madini).
Pia Manaibu Waziri wapya walioteuliwa ni Dk Seif Suleiman Rashid (Afya na Ustawi wa Jamii) na George Simbachawene (Nishati na Madini).
Wengine ni January Makamba Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia), Dk Charles Tizeba (Uchukuzi) na Amos Makala (Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo).
Manaibu Waziri wengine wapya ni Dk Binilith Mahenge (Maji), Stephen Maselle (Nishati na Madini), Angela Kairuki (Katiba na Sheria), Janet Mbene na Saada Mkuya Salum (Fedha).
Mawaziri waliobaki kwenye wizara zao:
Mabadiliko hayo hayakuwagusa baadhi ya mawaziri hivyo kuendelea kuzitumikia nafasi zao.
Mawaziri hao ni Stephen Wasira (Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Samia Suluhu (Ofisi ya Makamu wa Rais-Muungano), Dk Terezya Huvisa (Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira).
Wengine ni Mary Nagu (Ofisi ya Waziri Mkuu-Uwekezaji na Uwezeshaji), William Lukuvu (Ofisi ya Waziri Mkuu-Sera, Uratibu na Bunge), Samuel Sitta (Ushirikiano wa Afrika Mashariki), John Magufuli (Ujenzi) na Dk Shukuru Kawambwa (Elimu na Mafunzo ya Ufundi).
Mawaziri wengine ni Sophia Simba (Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto), Bernard Membe (Mambo ya Nje ya Ushirikiano wa Kimataifa) na Dk David Mathayo David (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi).
Wengine ni Gaudentia Kabaka (Kazi na Ajira), Makame Mbarawa (Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia) na Anna Tibaijuka (Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi).
Mawaziri waliobadilishwa wizara:
Rais Kikwete amewabadilisha wizara baadhi ya mawaziri, miongoni mwao na wizara walizohamishiwa kwenye mabano ni pamoja na Waziri wa Maji, Profesa Mark Mwandosya (Waziri asiyekuwa na wizara maalum).
Wengine ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-Tamisemi, George Mkuchika (Ofisi ya Rais-Utawala Bora), Waziri wa Katiba na Sheria, Celina Kombani (Ofisi ya Rais-Utumishi).
Pia yumo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utumishi), Hawa Ghasia ( Ofisi ya Waziri Mkuu-Tamisemi), Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa).
Wengine ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Ali Hassan Mwinyi (Afya na Ustawi wa Jamii) na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Mathias Chikawe (Katiba na Sheria).
Wengine ni Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni naMichezo, Emmanule Nchimbi (Mambo ya Ndani ya Nchi) na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Profesa Jumanne Maghembe (Maji).
Naibu Mawaziri waliopandishwa:
Kwenye orodha hiyo wamo Naibu Waziri waliopandishwa kuwa Mawaziri kamili katika wizara zao, akiwemo Christopher Chiza, (Kilimo, Chakula na Ushirika), Dk Fenella Mukangara (Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo).
Wengine waliopandishwa kwa kubadilishiwa wizara ni aliyekuwa Naibu Waziri Ujenzi, Dk Harrison Mwakyembe (Uchukuzi) na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Balozi Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii).
Naibu Mawaziri waliobaki kwenye wizara zao
Mabadiliko hayo hayakuwagusa baadhi ya Naibu Mawaziri akiwemo Dk Milton Makongoro Mahanga (Kazi na Ajira) na Benedict Ole-Nangoro (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi).
Wengine ni Mahadhi J Mahadhi (Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), Goodluck Ole-Medeye (Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi), Ummy Mwalimu (Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto).
Pia wamo Philipo Mulugo (Elimu na Mafunzo ya Ufunzi) na Abdalla Juma Abdulla (Ushirikiano wa Afrika Mashariki).
Naibu Mawaziri waliobadilishwa wizara:
Naibu Mawaziri waliobadilishiwa wizara zao ni Adam Malima (kutoka Nishati na Madini kwenda Kilimo, Chakula na Ushirika), Pereira Silima (kutoka Fedha kwenda Mambo ya Ndani ya Nchi na Gregory Theu (kutoka Fedha kwenda Viwanda na Biashara).
JK awavutia kasi watendaji wengine:
Wakati huo huo Rais Kikwete alisema uwajibishaji wa baadhi ya mawaziri, umefanyika kutokana na dhamana za kisiasa, lakini watendaji walioshiriki katika kashfa zilizipo kwenye taarifa zilizowasilishwa bungeni, watashughulikiwa.
“Kama ni shirika la umma, basi Ofisa Mtendaji Mkuu atawajibika, nitawaondoa watendaji wakuu waliotajwa kwa maana haiwezekani mawaziri peke wabebe mzigo wote wakati wahusika wengine wapo,” alisema.
Akasema watendaji hao ni pamoja na Makatibu wakuu, wakurugenzi mpaka bodi za mashirika ya umma wote hawako salama kufuatia kutimuliwa kwa mawaziri hao.
Asikiliza sauti za wabunge:
Akitangaza uamuzi huo na mabadiliko aliyofanya kwenye Baraza la Mawaziri Ikulu jijini Dar es Salaam jana, Rais Kikwete alisema hatua hiyo inatokana na mjadala uliofanyika bungeni na kutolewa mapendekezo ya kuwashughulikia mawaziri kadhaa, wakiwemo aliowakuza kazi.
Ubadhirifu wa mawaziri hao ulibainika kwenye ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Ludovick Utouh na ile ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira.
Hata hivyo, Rais Kikwete alisema baada ya majadiliano serikalini, ilibainika kuwa baadhi ya mawaziri hawakuhusika moja kwa moja na tuhuma zilizotolewa bungeni, hivyo kuwabadilisha wizara zao.
Ripoti zote zilisomwa wakati wa mkutano wa saba wa Bunge uliomalizika hivi karibuni mjini Dodoma, kiasi cha kuibua hisia za wabunge, wakitaka serikali iwashughulikiwe mawaziri hao.
Shinikizo la kushughulikiwa mawaziri hao lilichukua sura mpya pale Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe, alipowasilisha hoja ya Bunge kupiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Zitto alikusanya saini za wabunge zaidi ya 70 wakiwemo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), zinazotakiwa kwa mujibu wa kanuni za Bunge ili kupigwa kura hiyo.
Hata hivyo, kabla ya kuwasilishwa hoja ikiwa na na saini za wabunge, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alisema mchakato huo ulikuwa batili kwa vile haukikidhi kigezo cha kuwasilisha taarifa yenye saini hizo ndani ya siku 14 kabla ya kutolewa hoja husika.

No comments:

Post a Comment