Rais Jakaya
Kikwete amewafukuza kazi mawaziri sita waliotuhumiwa kukiuka maadili ya
utumishi na kushiriki ubadhirifu wa mali za umma.
Mawaziri hao na Wizara zao kwenye mabano
ni Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii), Cyril Chami (Viwanda na
Biashara) na Omar Nundu (Uchukuzi).
Wengine ni Dk Haji Mpanda (Afya na Ustawi
wa Jamii), William Ngeleja (Nishati na Madini) na Mustapha Mkulo
(Fedha).
Kwenye orodha ya waliofutwa kazi wamo
Naibu Mawaziri, Dk Lucy Nkya (Afya na Ustawi wa Jamii) na Athuman
Mfutakamba (Uchukuzi).
Mawaziri na Naibu Mawaziri wapya:
Kwa upande wa mawaziri wapya ni Dk
Abdallah Kigoda (Viwanda na Biashara), William Mgimwa (Fedha) na Profesa
Sospeter Muhogo (Nishati na Madini).
Pia Manaibu Waziri wapya walioteuliwa ni
Dk Seif Suleiman Rashid (Afya na Ustawi wa Jamii) na George Simbachawene
(Nishati na Madini).
Wengine ni January Makamba Mawasiliano,
Sayansi na Teknolojia), Dk Charles Tizeba (Uchukuzi) na Amos Makala
(Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo).
Manaibu Waziri wengine wapya ni Dk
Binilith Mahenge (Maji), Stephen Maselle (Nishati na Madini), Angela
Kairuki (Katiba na Sheria), Janet Mbene na Saada Mkuya Salum (Fedha).
Mawaziri waliobaki kwenye wizara
zao:
Mabadiliko hayo hayakuwagusa baadhi ya
mawaziri hivyo kuendelea kuzitumikia nafasi zao.
Mawaziri hao ni Stephen Wasira (Ofisi ya
Rais (Mahusiano na Uratibu), Samia Suluhu (Ofisi ya Makamu wa
Rais-Muungano), Dk Terezya Huvisa (Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira).
Wengine ni Mary Nagu (Ofisi ya Waziri
Mkuu-Uwekezaji na Uwezeshaji), William Lukuvu (Ofisi ya Waziri
Mkuu-Sera, Uratibu na Bunge), Samuel Sitta (Ushirikiano wa Afrika
Mashariki), John Magufuli (Ujenzi) na Dk Shukuru Kawambwa (Elimu na
Mafunzo ya Ufundi).
Mawaziri wengine ni Sophia Simba
(Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto), Bernard Membe (Mambo ya Nje ya
Ushirikiano wa Kimataifa) na Dk David Mathayo David (Maendeleo ya
Mifugo na Uvuvi).
Wengine ni Gaudentia Kabaka (Kazi na
Ajira), Makame Mbarawa (Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia) na Anna
Tibaijuka (Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi).
Mawaziri waliobadilishwa wizara:
Rais Kikwete amewabadilisha wizara baadhi
ya mawaziri, miongoni mwao na wizara walizohamishiwa kwenye mabano ni
pamoja na Waziri wa Maji, Profesa Mark Mwandosya (Waziri asiyekuwa na
wizara maalum).
Wengine ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu-Tamisemi, George Mkuchika (Ofisi ya Rais-Utawala Bora), Waziri wa
Katiba na Sheria, Celina Kombani (Ofisi ya Rais-Utumishi).
Pia yumo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais
(Utumishi), Hawa Ghasia ( Ofisi ya Waziri Mkuu-Tamisemi), Waziri wa
Mambo ya Ndani ya Nchi, Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga
Taifa).
Wengine ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa, Dk Hussein Ali Hassan Mwinyi (Afya na Ustawi wa Jamii) na
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Mathias Chikawe (Katiba na
Sheria).
Wengine ni Waziri wa Habari, Vijana,
Utamaduni naMichezo, Emmanule Nchimbi (Mambo ya Ndani ya Nchi) na Waziri
wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Profesa Jumanne Maghembe (Maji).
Naibu Mawaziri waliopandishwa:
Kwenye orodha hiyo wamo Naibu Waziri
waliopandishwa kuwa Mawaziri kamili katika wizara zao, akiwemo
Christopher Chiza, (Kilimo, Chakula na Ushirika), Dk Fenella Mukangara
(Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo).
Wengine waliopandishwa kwa kubadilishiwa
wizara ni aliyekuwa Naibu Waziri Ujenzi, Dk Harrison Mwakyembe
(Uchukuzi) na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Balozi Khamis
Kagasheki (Maliasili na Utalii).
Naibu Mawaziri waliobaki kwenye wizara
zao
Mabadiliko hayo hayakuwagusa baadhi ya
Naibu Mawaziri akiwemo Dk Milton Makongoro Mahanga (Kazi na Ajira) na
Benedict Ole-Nangoro (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi).
Wengine ni Mahadhi J Mahadhi (Mambo ya
Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), Goodluck Ole-Medeye (Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi), Ummy Mwalimu (Maendeleo ya Jamii, Jinsia na
Watoto).
Pia wamo Philipo Mulugo (Elimu na Mafunzo
ya Ufunzi) na Abdalla Juma Abdulla (Ushirikiano wa Afrika Mashariki).
Naibu Mawaziri waliobadilishwa
wizara:
Naibu Mawaziri waliobadilishiwa wizara
zao ni Adam Malima (kutoka Nishati na Madini kwenda Kilimo, Chakula na
Ushirika), Pereira Silima (kutoka Fedha kwenda Mambo ya Ndani ya Nchi
na Gregory Theu (kutoka Fedha kwenda Viwanda na Biashara).
JK awavutia kasi watendaji
wengine:
Wakati huo huo Rais Kikwete alisema
uwajibishaji wa baadhi ya mawaziri, umefanyika kutokana na dhamana za
kisiasa, lakini watendaji walioshiriki katika kashfa zilizipo kwenye
taarifa zilizowasilishwa bungeni, watashughulikiwa.
“Kama ni shirika la umma, basi Ofisa
Mtendaji Mkuu atawajibika, nitawaondoa watendaji wakuu waliotajwa kwa
maana haiwezekani mawaziri peke wabebe mzigo wote wakati wahusika
wengine wapo,” alisema.
Akasema watendaji hao ni pamoja na
Makatibu wakuu, wakurugenzi mpaka bodi za mashirika ya umma wote hawako
salama kufuatia kutimuliwa kwa mawaziri hao.
Asikiliza sauti za wabunge:
Akitangaza uamuzi huo na mabadiliko
aliyofanya kwenye Baraza la Mawaziri Ikulu jijini Dar es Salaam jana,
Rais Kikwete alisema hatua hiyo inatokana na mjadala uliofanyika bungeni
na kutolewa mapendekezo ya kuwashughulikia mawaziri kadhaa, wakiwemo
aliowakuza kazi.
Ubadhirifu wa mawaziri hao ulibainika
kwenye ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali,
Ludovick Utouh na ile ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na
Mazingira.
Hata hivyo, Rais Kikwete alisema baada ya
majadiliano serikalini, ilibainika kuwa baadhi ya mawaziri hawakuhusika
moja kwa moja na tuhuma zilizotolewa bungeni, hivyo kuwabadilisha
wizara zao.
Ripoti zote zilisomwa wakati wa mkutano
wa saba wa Bunge uliomalizika hivi karibuni mjini Dodoma, kiasi cha
kuibua hisia za wabunge, wakitaka serikali iwashughulikiwe mawaziri hao.
Shinikizo la kushughulikiwa mawaziri hao
lilichukua sura mpya pale Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto
Kabwe, alipowasilisha hoja ya Bunge kupiga kura ya kutokuwa na imani na
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Zitto alikusanya saini za wabunge zaidi
ya 70 wakiwemo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), zinazotakiwa kwa mujibu wa
kanuni za Bunge ili kupigwa kura hiyo.
Hata hivyo, kabla ya kuwasilishwa hoja
ikiwa na na saini za wabunge, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alisema
mchakato huo ulikuwa batili kwa vile haukikidhi kigezo cha kuwasilisha
taarifa yenye saini hizo ndani ya siku 14 kabla ya kutolewa hoja husika.
No comments:
Post a Comment